juu

Wednesday 11 December 2019

Majukumu ya mke na mume ndoani

Must Follow Relationship Rules For Happy Love

Ndoa ni haja ya kawaida kwa kila mwanadamu. Ndoa ndio njia pekee ya kujenga familia, ndoa ndio njia halali ambayo binadamu yeyote anaruhusiwa kutimiza haja zake kimwili tofauti na hapo…. Kwani Mwanaume ameubwa kwa ajili ya mwanamke hali kadhalika mwanamke ameubwa kwa ajili ya mwanaume “Bwana Mungu akasema si vema huyu mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye, Bwana Mungu akamletea Adam usingizi, naye akalala; kisha akatwaa ubavu mmoja, akafunika nyama mahali pake, na ule ubavu alioutwaa katika Adam Bwana Mungu akaufanya mwanamke, akamleta kwa Adam; kwa hiyo mwanaume atamwacha baba yake na mama yake ataambatana na mkewe na watakuwa kitu kimoja (Mwanzo 2:18…..24)

Lakini kwa sasa hakuna suala gumu, tata na nyeti linalohusu maisha ya watu kama ndoa. Kumekuwa na migongano mingi na mizozo isiyo kwisha katika maisha ya ndoa. Leo ndoa imeonekana kama utumwa, mzigo au kubebeshwa msalaba, na sasa imekuwa kawaida watu kufunga ndoa saa sita mchana kufika saa 12 jioni ndoa imevunjika. Tena jamii yetu ya sasa iliyomomonyoka maadili na kuingiliwa na utamaduni wa kimagharibi ndio kunachangia zaidi migogoro na mivutano katika ndoa.

Kumekuwa na mada nyingi humu zinazohusu ndoa, wengine kuumizwa katika ndoa, wengine kusalitiwa, kupigana mpaka kutoana manundu, wengine hata kuana na wengine kuachana kabisa. Ndio maana nimeona nilete mada hii mezani tuijadili kwa mapana pamoja.

Kwa kuanza kwangu kuchangia katika mada hii nitajikita kuelezea majukumu ya mke kwa mume wake na majukum ya mume kwa mke wake. Kwa sababu kila mtu anayeingia katika mkataba wa ndoa, anaingia katika mkataba huo akiwa na matatizo yake binafsi na kiasi fulani cha ujinga wake. Ili ndoa iweze kustawi na kudumu lazima kila mwanandoa ajue wajibu na majukum yake. Wahenga wanasema ndoa ni chuo, hivyo wanandoa wanashauriwa kuwa tayari kujifunza, ndoa haiwezi kuimarika endapo wanandoa hao watabaki kung’ang’ania misimamo yao waliyokuwa nayo kabla ya kuona. Na hizi ndio njia pekee za kuimarisha na kustawisha ndoa na kuwa ya furaha wakati wote. naelezea kwa ufupi ili nisimchoshe msomaji.

Nikianza na majukumu ya mke kwa mume wake:

(1) Kazi ya mke ni kumtunza na kumlea mume. Najua hii si kazi rahisi kwa wanawake wengi, jukumu hili linahitaji busara, hekima na mbinu nyingi.

(2) Kumstahi na kumheshimu mume . kumheshimu mume wako haina maana umejidhalilisha, Bali njia ya kuonyesha upendo kwake na unamjali. Unatakiwa uwe mpole na adabu unapozungumza na mume wako, usizungumze nae kwa ukali, usimtukane, uwe msikivu kwake wakati wote. Tena usithubuti kumwita mume wako majina machafu au majina ya utani asiyoyapenda. Mumeo anapokuja nyumbani, jaribu kutabasam na kumsalimia kwa uchangamfu. Sio akifika umefura kama umemeza chura. Hapo unampa nafasi ya kuchepuka tu, akafurahie nyumba ndogo maana akifika mlangoni tu ameishaitwa majina 40 kidogo tena matamu, anapokelewa kwa mabusu na mahaba ya hali juu, kisha anavulishwa kiatu na nguo na kutengewa maji ya moto ya kuoga. Mwisho wa siku anaamia nyumba ndogo we unabaki unalalama tu mme wangu kalishwa libwata wapi kaa hapo.

(3) Epuka malalamiko na manung’uniko. Ni kweli hakuna mtu asiye kuwa na matatizo na manung’uniko kuhusu maisha. Lakini kuna baadhi ya wanawake wao kutwa malalamiko hasa yanayolenga maisha ya kipato cha mume na watu wengine. Muda wote mbona Mimi unajanunulia hiki, mbona yule ana hiki, tena analalamika bila kujali uwezo wa mume. Inafika mahali mwanaume anakata tamaa, maana tabia ya mwanamke kulalamika, kunung’unika na kudekadeka wakati wote inaudhi wanaume wengi.

(4) Kuwa mvumilivu wa kazi ya mume wako. Kila mtu anayo kazi na kazi zimetofautiana, na kila kazi ina hadha yake. Kama mume wako ni Mwalimu, daktari, dereva, mhandisi, fundi ujenzi, fundi makanika, muokota makopo n.k ipende kazi yake na umshukuru Mungu kwamba mume anajishughulisha. kwa mfano Daktari ukesha hospitalini akiwahudumia wagonjwa, Dereva husafiri sana na kutumia siku kadhaa kuwa mbali na nyumbani kwake. Mwalimu anatumia muda wake mrefu kutayarisha masomo, kusahihisha kazi za wanafunzi. Fundi makanika, kutwa nzima anachezea mafuta machafu na grisi, na wafanyakazi wengine hali kadhalika.

Shida inakuja mwanamke anataka mume awe nyumbani mapema na matatizo kwa wale wanaoishi Dar foleni, basi mume akifika nyumbani tu basi mke anamudandia ulikuwa kwa mahawara wako na maneno mengine ya maudhi. Bahati mbaya sana kuna wengine wanakuwa sio waaminifu kwenye ndoa zao kutokana na kazi ya mume kwa mfano km madereva wa masafa marefu dah! Ngoja niachie hapo lakini huo nimetolea mfano tu madereva msije mkanitoa nyongo bure.

(5) Usiwe na tabia ya kumwazia mume wako vibaya. Tabia ya kumwazia mwenzako vibaya ni tabia mbaya sana tena yenye madhara makubwa. Bahati mbaya wanawake wengi wana ungojwa huu. Si vibaya kumfatilia mume wako lakini tabia hii isivuke mipaka. Ukiona mwanamke mwenzako kamchangamkia mume wako au kumsalimu tu basi ni hawara yake, akitoa msaada wowote kwa mwanamke yeyote hata kama ni mjane, unasema sio bure kuna namna hapa unafura, Akimpa lifti mwanamke yoyote hata kama ni bibi kizee utasikia siku hizi unachukua mpaka vibibi Mimi sikuridhishi?

Mwanamke yoyote akimsifia mume wako jamani ana roho nzuri, mkarimu na mpole basi inakuwa tabu kwa mumeo siku hiyo apakaliki ndani. Ukisikia simu ya mumeo inaita unakimbia kwenda kusikiliza anaongea na nani, meseji ikiingia unataka uwe wa kwanza kusoma. Kila saa mume anakaguliwa. Kwa tabia kama hizi huifanya nyumba kuwa jehanamu kwa mume. Nyumbani panakuwa pachungu kuishi.

(6) Mwanamke unatakiwa kutunza siri za mumeo. Wanaume wengi wanaamini wanawake awawezi kutunza siri. Ni kweli wanawake wengi wanapenda kutoa siri za ndani sana na kupeleka kwa marafiki na majirani. Japo wanawake wengi wanapenda kujua siri za mume wake, lakini wanaume hawako tayari kuwambia siri zao kila kitu. Unapotaka kujua siri za mume wako jifunze kutunza siri.

Sifa nyingine kwa ufupi, kubali uongozi wa mume wako hata kama una PhD 3, una mamlaka makubwa serikalini usije kuyaleta kwa mumeo, hayo mamlaka yako yaishie getini. Uwe safi na Mrembo muda wote huwapo nyumbani sio kujiachia tu, na wengine mawingi kichwani mpaka yanatoa harafu, jumlisha na kikwapa mume lazima akimbie tu.

Unatakiwa umrizishe mume wako na si wazazi wako. Uwe mwelevu na mvumilivu pale kipato kinapoyumba. Epuka kushiriki kupiga umbea. Kuna sifa nyingi lakini ngoja niwaachie wengine muendeleze.

Kwa upande wa Mume:

(1) Mume ni mlinzi na mlezi familia. Wajibu mkubwa wa mwanaume katika ndoa ni kulea na kutunza familia(Kichwa cha familia). Kwa ufupi.

(2) Mpende mke wako. Mke wako kabla ya kumuo alikuwa anafaidi mapenzi toka kwa wazazi wake, sasa ameamua kuingia katika mkataba wa ndoa na wewe, kuishi maisha yake yote basi mpende sana. Kumuoa mwanamke sio kumuajiri kama mfanyakazi, bali ni kumchagua mwenza na rafiki ambaye utaishi naye katika maisha yako yaliyosalia.

Sifa zingine kwa ufupi:

Mtumze mke wako, usipomtunza usije kulauumu kutunziwa na wanaume wa mjini. Kuwa mfariji na kumliwaza mke wako kila wakati unapopata nafasi. Epuke kutafuta mapungufu kwa mke wako. Epuka kusikiliza maneno ya pembeni. Usitamani wanawake wengine. Uwe na shukrani kwa mkeo. Na sifa nyingine nyingi.

Lakini sifa kubwa kuliko zote: Kwa imani ya dini zetu mumtangulize Mungu kila wakati ombeni na mumlilia kwa ajili ya ndoa yenu, hakuna mtu atakayefurahi mkiishi kwa amani na mumeo au mkeo, wataanzisha fitina na kuwaendea hata kwa sagoma muachane. Lakini wanaomwamini Mungu hayatawapata kamwe mtazidi kuimarisha zaidi penzi lenu na kuwa la furaha.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Translate

sam magelle

Main Menu Links

HABARI KALI ZAIDI

HABARI ZILIZOPITA

CHAGUA HABARI na sammagelle.com

Copyright © juu | Powered by Blogger