juu

Wednesday 18 December 2019

Ukitegemea Kupata Kitu Penzi Utaliona Chungu.



Si jambo la kushangaza kuwaona au kusikia mwanamke na mwanaume wanapendana. Yaani kila mmoja anampenda mwenzake na hivyo kuanzisha uhusiano.

Hapa nazungumzia upendo wa umoja na si wa wingi. Yaani wale wanaopendana huku kila mmoja akiwa hana mwenza mwingine. Inapotokea mtu ana mwenza halafu akapenda kwingine, huo ni usaliti na si mada yangu ilipolalia wiki hii.
MADA YENYEWEMada yangu inajieleza hapo juu; ukitegemea kitu penzi utaliona chungu.
Wapo watu ambao wanaingia kwenye mapenzi kwa sababu ya kupenda kutoka kwenye sakafu ya mioyo yao. Yaani mfano, mwanamke anatokea kumpenda mwanaume fulani pasipo na sababu yoyote. Huo ndiyo upendo unaoitwa wa dhati!

Lakini wapo wanaopenda kwa sababu ya kitu. Mfano, mwanamke anatokea kumpenda mwanaume kwa sababu ana gari, ni msomi, ana pesa, ni mfanyabiashara, ana cheo serikalini, ni staa wa mpira wa miguu, ni mwimbaji mzuri wa Bongo Fleva au ana umaarufu sana mitaani.
HATA MBWEMBWE ZINA UPENDO?
Katika hili, nimewahi kushuhudia dereva wa bodaboda akipendwa na msichana kwa sababu tu ya uendeshaji wake wa bodaboda mitaani. Akiingia watu wanajua huyo ni Yusuf kwani mlio mkubwa, mwendo kasi akiwakwepa watoto wa mitaani, honi nyingi, breki za ghafla, sehemu nyembamba anapita kwa spidi na watu wanamsema vibaya kila siku; ‘huyu Yusuf huyu, iko siku.’

Kwa tabia hiyo tu, msichana mmoja aliondokea kumpenda sana Yusuf. Nilibaini hilo kwani Yusuf alipokuja kunyang’anywa pikipiki na bosi wake akawa hana mbwembwe tena na uhusiano wake na yule msichana ukafa.

Yusuf hakuwa na pesa za kumhonga huyo msichana, kwani yeye alikuwa akifanya biashara zake, sanasana yeye Yusuf ndiye aliyekuwa akipigwa tafu ya vijisenti.
LAKINI KUNA KUNDI HILIKundi ninalopenda kulizungumzia kwa leo ni lile la wanawake hasa, ambao wanaingia kwenye uhusiano wa kimapenzi na wanaume kwa dira zao.

Utakuta mwanamke anamkubali mwanaume kwa sababu tu amehisi atakuwa akipewa pesa nyingi. Au kama mwanaume ana duka, anategemea akimkubali atakuwa akipewa bidhaa za dukani bure.

Wengine ni wale wanaoingia kwenye uhusiano kwa sababu wanaume hao wana vyeo vikubwa au ni mastaa, hawa ndiyo ninaosema mimi kwamba, inapotokea pesa zimekata, hapewi kama zamani, inapotokea cheo kimeisha, inapotokea hali ya biashara inayumba hivyo hapewi mchele kama zamani ndiyo hujuta na kuliona penzi ni chungu.
KUWA KATIKA KUNDI HILISiku zote unapotaka kuingia kwenye uhusiano kubali kwa mwanaume ambaye kila ukipima upendo wako kwake unauona hauna sababu yoyote. Yaani humpendei pesa, humpendei cheo wala ustaa, bali unampenda tu! Ndiyo maana wahenga walisema penye penzi la kweli, mwenye chongo huonekana ana makengeza!

Ukipenda kwa mtindo huu, huwezi kuteseka kwani hali yoyote utakubaliana nayo.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Translate

sam magelle

Main Menu Links

HABARI KALI ZAIDI

HABARI ZILIZOPITA

CHAGUA HABARI na sammagelle.com

Copyright © juu | Powered by Blogger